Saturday 21 July 2012

RINDA FUPI NI HALALI!

Waziri wa Elimu mheshimiwa Mutula Kilonzo amejitokeza bayana kuwaunga mkono wanafunzi waliogoma wakidai wanalazimishwa kuvaa marinda marefu zaidi....Akasema kuwa hata sketi likiwa fupi halina shida kwani watoto si "watawa!"..........Kwa muktadha huo nikalitunga shairi "kuusifu" uamuzi huu wa kipekee!

WAZIRI AMEPITISHA
Kalamu na karatasi, n'andike hili kwa kasi,
Nimimine zangu hisi,niseme zangu tetesi,
Nimpongeze farisi,nimpe kongole sisisi,
Waziri ametangaza,marinda yapande juu.

Nimependezwa hakika, ni uamuzi mwafaka,
Rinda refu ni dhihaka,kwa nchi 'loimarika,
Minofu ikifichuka,ishara "tumechanuka"
Waziri amekubali, wana wakude marinda.

Rinda hadi aridhini,halifai aswilani,
Fedheha kubwa shuleni,waziri amebaini,
Rinda refu ni la nini, kuvaliwa darasani?
Waziri amepitisha,nani wewe kuipinga?

Kidete amesimama,jukwaani akasema,
Rinda refu si salama,ni bovu tena la zama,
Fupi linalo heshima,halitazua zahama,
Waziri amepitisha,watoto wavae mini.

Binti zetu si watawa,hawafai kuonewa,
Wana uhuru kwamuwa,wapewe hino satuwa,
Tuache kuwaumbuwa,kuwashikia shokowa,
Waziri amekubali, tuvae tunavyotaka.

Kenya imeendeleya, usasa kukumbatiya,
Haifai kubakiya,nyuma mithili mikiya,
Hata mini kivaliya,wana hawana hatiya,
Mutula amepitisha,sketi refu si njema.

Mutula nakupongeza,wana 'mewatelekeza,
Wazo lako lapendeza,wizara waendeleza,
Mambo unayageuza,uzidi kutuongoza,
Waziri amepitisha, rinda fupi ni halali.

Totauti siioni,darasa na danguroni,
Kama si uhayawani, basi nambie ni nini,
Kilichobaki ni nini,Mutula tuelezeni?
Waziri amepitisha, darasa liwe danguro!

Mwisho ninahitimisha,kololo nimedondosha,
Musere ninafungasha,uyumbe 'mewasilisha,
Mutula yuatamausha,wazazi 'megadhabisha,
Waziri amepitisha,wana wavae kihuni.
        SOLOMON OLE MUSERE,
        Chuo kikuu cha Kenyatta,
            NAIROBI.
        21 Julai 2012

MOLA NITAKUTUKUZA

Waama, yote aliyonitendea Mungu siwezi kuyahesahu moja kwa moja.Beti zifuatazo zinajaribu kutaja japo baadhi ya mema na makuu aliyonitendea Maulana.

MOLA NINAKUTUKUZA:
Ninapanda jukwaani,nimhimidi Manani,
Nyingi swifa za yakini,zinitokazo moyoni,
Ndiye wangu tumaini, kimbilio maishani,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.

Umenipa afya njema, mie sina hata homa,
Umenitunza Karima,muweza mwenye rekhema,
Umenepusha zahama, isinipate tuhuma,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.

Kisomo 'menijaliya, nasoma bila udhiya,
Karo wanigharamiya, kwa wema wako Jaliya,
Motisha 'menipa piya,nipate kuendeleya,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.

Kila siku twasikiya, ajali zimetokeya,
Roho zimeangamiya, na majuruhi mamiya,
Haya umenepushiya, kwa neemayo Jaliya,
Mola ninakutukuza,kwa yote lonitendea.

Vitendo vya kihalifu,nchini kwetu sufufu,
Maafa ni maradufu,kila kutwa yasadifu,
Pasipo wewe Raufu, mie ningekuwa mfu,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.

Nikupe nini muweza, hidaya ya kupendeza?
Nimejaribu kuwaza, kuipata sijaweza,
Wemawo wa kushangaza, popote nitangaza,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.

Daima humithiliki,Rabana msitahiki,
Ewe ndo wangu rafiki,kwenye faraja na dhiki,
Daima hunigeuki, Jalia mpenda haki,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.

Mikono na'kwinulia,kwako ninakimbilia,
Zaburi nita'kwimbia,kinywani mwangu Jalia,
Katu sitanyamazia, makuu 'lonitendea,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.

Rabana uhimidiwe, jinalo libarikiwe,
Kwa swifa ushangiliwe,kwa nderemo hata shangwe,
Magoti na upigiwe,kwa dua usujudiwe,
Mola ninakutukuza, kwa yote 'lonitendea.

Ukingoni nimefika, shairi 'metamatika,
Namshukuru Rabuka, Muumba aloswifika,
Utulinde mtukuka, tupate kuneemeka,
Mola ninakutukuza, kwa yote lonitendea.
SOLOMON OLE MUSERE,
Chuo kikuu cha Kenyatta,
      11 Julai 2012



KONGOLE WANASIASA

Kwa moyo wa kujituma, najitolea mhanga kama mhanga kuisifia dhima sheshe wanayotekeleza wanasiasa wetu hasa hao wanaowania urais kwenye uchaguzi ujao.Nani kama wao!

KONGOLE WANASIASA
Hewaa ndugu hewaa,lau kipungu napaa,
Nangia bila fadhaa,kwa beti ziso mawaa,
Tega lako lau paa,tuwaswifu mashujaa,
Kongole wanasiasa,mafundi wa kutongoa.

Mafundi wa kutongoa,wasemi waso na doa,
Kalima mwazishopoa,kokote mnapotua,
Ahadi chekwa mwatoa, nyingine za kushitua,
Kongole wanasiasa,farisi walobobea.

Farisi walobobea,waama nawaswifia,
Kofia nawavulia,si shere nawachezea,
Kokote mwatuchochea, fulani kumchukia,
Kongole wanasiasa,walumbi wenye busara.

Walumbi wenye busara,na bonge la mishahara,
Japo nchi ni fukara,dhima yenu bar'abara,
Uchumi umedorora,'meadimika ajira,
Kongole wanasiasa,wakenya twawathamini.

Wakenya twawathamini,'tawarejesha bungeni,
'Tawatetea debeni,wangwana waso kifani,
Japo twala mapipani,pasi kivazi milini,
Kongole wanasiasa,wajumbe wasitahiki.



Wajumbe wasitahiki, nani atawadhihaki?
'Metuondelea dhiki,japo 'meinajisi haki,
Matendo yenu afiki, na ndimi tamu ja uki,
Kongole wanasiasa,maneno yenu matamu.

Maneno yenu matamu, mithili ya zamzamu,
Farisi wa kushitumu,kwa tenzi za kuhujumu,
Wajumbe nawaheshimu,japo ndimi zenu sumu,
Kongole wanasiasa,kusema kweli mwayuwa.

Kusema kweli mwayuwa,ahadi kuzipomowa,
Jukwaani mkituwa,wakata tunachachawa,
Viuno 'twavinenguwa, tuisahau shakawa!
Kongole wanasiasa, kipaji bora mnacho.

Mnacho bora kipaji,namshukuru mpaji,
Nawavisheni mataji,nimalize utungaji,
Sinione mjuaji,nguchiro mkosoaji
Kongole wanasiasa, kwa bora wenu 'wongozi.

Kikomo ninakomile,uyumbe 'meupatile,
Ziada siandikile,'nisije fumwa mishale,
Virago nafungatile,mwituni nijitomile,
Kongole wanasiasa,kwa sheshe wenu wajibu.
        SOLOMON OLE MUSERE,
        Chuo kikuu cha Kenyatta,
            NAIROBI.
            17 Julai 2012.   

Tuesday 29 May 2012

NAMTAFUTA KIDOSHO

PENZI LA DHATI

Bisimillahi  Rabuka,  illahi   Mola  muweza,
Mwanao nalalamika, upweke menilemaza,
Jamani  nahuzunika,nani tanituliza?
Namtafuta kidosho,  mwenye penzi la hakika.

Asiwe mwenye papara,ninachelea chiriku,
Kimwana wa hapa bara, mgeni nitamshuku,
Kidosho mwenye busara, asokuwa zumbukuku,
Namtafuta kidosho, mwenye penzi la hakika.

Ninamsaka tabibu, alo na mwingi mahaba,
Yangu roho aitibu, kwa mapenzi yaso haba,
Awe wa kwangu swahibu, upweke umenikaba,
Namtafuta kidosho, mwenye penzi la hakika.

Awe  na  bora umbile, na twabia adilifu,
Mtoto mwenye sumile,mwenye haiba faafu,
Nitalivaa penzile,  shingoni  lau mkufu,
Namtafuta  kidosho, mwenye penzi la hakika.

Nitamtwika jukumu, yangu roho kutuliza,
Ashike  hino hatamu, rohoni kuniliwaza,
Maneno yake matamu,upweke kuifukiza,
Namtafuta  kidosho, mwenye penzi la hakika.

Awe na mwingi heshima,  kwa wadogo na wakubwa,
Kimwana mwenye hekima, asiyetokwa ubwabwa,
Alo tayari kwa dhima, kutenda yalo makubwa,
Namtafuta  kidosho, mwenye penzi la hakika.

Atanituza  Rabana, tunda la roho yangu,
Matoni nikimuona, yatanitoka matungu,
Hakika tutapendana, malaika ua langu,
Namtafuta kidosho, mwenye penzi la hakika.

Kaditama wa tamati,kalamu ninailaza,
Wazo langu siliati,narudia kutangaza,
Khaherini mabenati, dhima hino mewatweza,
Namtafuta kidosho mwenye penzi la hakika.

SOLOMON OLE MUSERE
CHUO KIKUU CHA KENYATTA
2011.

Friday 11 May 2012

ULIYATAKA MWENYEWE

ULIYATAKA MWENYEWE,
Mrembo  nakuswabahi,natumai u buheri,
Fursa hino  naiwahi, kukuasa kishairi,
Nanena yalo sahihi,nikwambile  pasi siri,
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?

Kidosho nilikupenda,posa nikakuletile,
Nawe juu ukapanda,kuwa mie mchochole,
Nenda basi mwanakwenda, Musere nikakwambile
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?

Bwanyanye kakughilibu,ukawa windo rakhisi,
Ukalikumbatia dubu, kwa tamaa ya ukwasi,
Kirinda pasi aibu, kikakutoka kwa kasi,
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?

Mhuni ukampa fursa, lako tunda kulimega,
Mkazamia anasa, mahaba yaliponoga,
Kila siku kawa misa, kokote mkijibwaga,
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?

Dunia hutoiweza, nilikupa mausiya,
Matusi 'kanilekeza, kisema nakuchongeya,
Ukajigeuza pweza, makaa kujipaliya,
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?

Hakika niliumiya,kimwana ulipozama,
Mengi nilokutendeya, ukaleta uhasama,
Kabidi kunyamaziya,kwa soni nikiinama,
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?

Haikupita miezi, akakuponyoka Keni,
Likavuruga penzi, kitumbua mchangani,
Ukaachwa na matozi, na ndwele humo mwilini
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?

Katu huoni fedheha, eti wajileta kwangu?
'Sitaraji msamaha, hilo muuze Mungu,
Ulotenda ni karaha,yalinitia utungu,
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?

Kikomo ninapotia, kidosho ushasikia,
Katu sitochelea,ukweli kukuambia,
Hilo kero fikiria, ndo ujumbe nakuatia,
Uliyataka mwenyewe, na sasa kilio chani?

SOLOMON MUSERE, FEB 2012.
CHUO KIKUU CHA KENYATTA

Monday 19 December 2011

MITIHANI SI HUKUMU!

Beti zifuatazo, nilitunga ili kuwapa moyo na kuwatakia kila lenye kheri na fanaka watahiniwa wote nchini wa darasa la nane walipokuwa wakiusubiri mtihani wa kitaifa wa K.C.P.E  Mwaka huu, 2011.

NASAHA ZA MITIHANI.
Ngu'zangu sabalkheri, nimerejea tungoni,
Naja kwenu na urari, ya nasaha niwapeni,
Ninalo wazo kitwani, naomba niwajuzeni,
Mitihani si janga, ni kigezo cha ubora.


Jambo hili si khiari, mitihani kufanyeni,
Lahitaji ujasiri, wanakwetu jikazeni,
Ufanisi kushamiri, bora uwe na makini,
Mitihani si maafa, ni kigezo cha ubingwa.


Yafaa uwe na ari, mja mwenye tumaini,
'Sianze kutahayari, ni bora ujiamini,
Hakikisha u tayari, ufikapo ukumbini,
Mitihani ni daraja, itakuvusha majini.


 Mitihani ni safari, huepuki maishani,
Watazame wahadhiri, mawakili na rubani,
Wote hao watakiri, walifanya mitihani,
Mitihani ndiyo dira, na ramani maishani.


Nawapeni tahadhari, 'sijipate taabani,
Maswali uyafasiri, usijitie mbioni,
Pupayo takuathiri, mitihani ukafeli,
Mitihani si adhabu, apewayo baradhuli.


Soma swali ubashiri, hoja zake mtahini,
Soma kila mistari, upitie kwa makini,
Hatiyo iwe nzuri, isiwe na walakini,
Mitihani ni mwongozo, kufikia ubingwani.


Usijiole mahiri, mitihani si utani,
Si vema kuwa jeuri, hamna maswali duni,
Mambo yote huwa shwari, kitulia akilini,
Mitihani si pigo, ni faraja kwa mweledi.


Watahini ni mahiri, watungapo mitihani,
Si rakhisi kubashiri, na mitego kubaini,
Yao nia si dhahiri, utadhani 'mahaini',
Mitihani si mzaha, sharti uwe na makini.


Kiamka alfajiri, piga dua kwa Manani,
Akuepushie shari, akili ziwe razini,
Atawatuza Khahari, hawaati abadani,
Mitihani si hukumu, ni hidaya za jamala .


Kaditama ninakiri, kwenda mbee sitamani,
Nawombeeni kheri, na fanaka maishani,
Atawapeni buheri, aloswifika Manani,
Mitihani ndiyo ngazi, kufikia kileleni.

Solomon ole Musere ,
Chuo kikuu cha Kenyatta
Nov 2, 2011

PUNGUZENI VIPODOZI

Hakika inavunja moyo kuona jinsi wengi wetu tunavyopenda kutumia vipodozi, kiasi cha kuifuja ngozi, uzuri na haiba ya kipekee tuliojaliwa na Muumba! Naam, si vibaya kujipodoa, lakini ukizidisha basi unajipunguzia uzuri, mvuto na  isitoshe,kuivuruga haiba ya wajihi na hadhi  yako pia!
TUTHAMINI "UREMBO WA KIWETU!"

PUNGUZENI VIPODOZI.
Kuna tendo lanighasi, nilionalo ni hasi,
Linaibua utesi, na hisia za uasi,
Ninalipinga kwa kasi, natangaza wasiwasi,
Punguzeni vipodozi, vinapunguza  haiba.

Ninashindwa kutambua, kwanini mwajiumbua,
Hili swala lazuzua, natamani kung'amua,
Nawaza nikiwazua, kamwe sijalitambua,
Punguzeni vipodozi, vinapunguza haiba.

Silika ino'chukiza, kulla jambo kuigiza,
Tuliumbwa kupendeza, kwanini twajichakaza?
Yafaa kumtukuza, Muumba alo Muweza,
Punguzeni vipodozi, vinapunguza haiba.

Ewe binti mwafrika, tizama 'livyoumbika,
Urembo wa malaika, kokote watamanika,
Weusi ulioshika, hakika unapendeka,
Punguzeni vipodozi, vinapunguza haiba.

'Mepewa ngozi laini, nyororo iso kifani,
Ukaona haifani, alivyoumba Manani,
Ukajifuja kwa kani, vipodozi kusheheni,
Punguzeni vipodozi, vinapunguza haiba.

Vipuli masikioni, na mikufu ya shingoni,
Mwajitoga sikioni, utungu kujitieni,
Wekundu wa mdomoni, ni upi wake thamani ?
Punguzeni vipodozi, vinapunguza haiba.

Kuchazo mwapaka hina, mkidhani mtafana,
Nyengine ni ndefu sana, zatisha ukiziona,
Umuonapo kimwana, mhanga amefanana!
Punguzeni vipodozi, vinapunguza haiba.

Rangi hino maozini,thamani katu sioni,
'Kivaa vingi vipini, uzuri kamwe hunani,
Ndonya 'kitia puani, watangaza jambo gani?
Punguzeni vipodozi, vinapunguza haiba.

Tisa beti timilifu, hatima imesadifu,
Musere nakuarifu, ufate nyendo 'faafu,
Tuzidi kujinadhifu, apendavyo Mtukufu,
Punguzeni vipodozi, vinapunguza haiba.

SOLOMON OLE MUSERE,
'Malenga mwitu'
CHUO KIKUU CHA KENYATTA.

Friday 16 December 2011

SI'BAGUE MLEMAVU

SI'BAGUE MLEMAVU

Nawaswabahi wendani,salamu zipokeeni,
Nawasihi sogeeni, na masikio nipeni,
Majibu kisha nipeni, nifikapo hatimani,
Sibague mlevavu, kwani mja mwenzako.

Mlemavu mwenye baa, ni yule mwenye kichaa,
Kwani awapo na njaa, hula hata kwenye jaa,
Huzua kubwa balaa, hatulii akakaa,
Si'bague mlemavu, kwani  mja mwenzako.

Aweza kuwa kipofu, subiri nikuarifu,
Akawa ni maarufu,kutunga nyimbo sanifu,
Ni mtunzi msarifu, lugha bora na faafu,
Si'bague mlemavu, kwani mja mwenzako.

  Kiwete hana miguu, japo hutenda makuu
Kazini 'tapanda juu, kushinda wenye miguu,
Watakuita mkuu, pasi na yako miguu,
Si'bague mlemavu, kwani mja mwenzako.

Ulemavu si kikwazo, kisiasa na michezo,
Mlemavu ana uwezo, kuongoza bila bezo,
Tamasha na tumbuizo,'takutia chachawizo,
Si'bague mlemavu, kwani mja mwenzako.

Japokuwa ni kiziwi,anao bora ujuzi,
Dosari katu hatiwi, taitwa hata mjuzi,
Daima habaguliwi,haina doa uziwi,
Si'bague mlemavu, kwani mja mwenzako.

Kuna wengi washairi, malenga walo mahiri,
Tungo zao mashuhuri, watunzi waso kiburi,
Zao tungo ni johari, zaonya na kushauri,
  Si'bague mlemavu, kwani mja mwenzako..

Hatima hapa natuwa, wangu wosia 'metowa,
Mlemavu kumbaguwa, mwenyewe wajiumbuwa,
Kikomoni ninatuwa, hili jamvi  nakunjuwa,
Si'bague mlemavu, kwani mja mwenzako.


Solomon ole Musere.
Chuo kikuu cha Kenyatta
       2011

UA LANGU.

WARIDI WANGU
Kamwe sifanyi ajizi, kalamu nakumbatiya
Ya muhimu maongezi, sitaki kukiakiya,
Umenikoleza penzi, nazunguka kama piya,
Ua langu la waridi, ninakuenzi kimwana.

Ewe ni jizi mahiri, uloiba cha thamani,
Meinyakuwa suduri, na mawazo matekani,
Bila soni nakariri, nimebaki kifungoni,
Ua langu la waridi, ninakuenzi kimwana.


Moyoni sina terema, kiwa mbali na waridi,
Malaika husimama, nikumbukapo miadi,
Malaji hayawi mema , upweke kweli hasidi,
Ua langu la waridi, ninakuenzi kimwana.

Popote nikitembeya , sitakuacha mahabubu,
Pichayo mejibebeya, mapuzi yasinisibu,
Moyini mekufichiya, uwe wangu taabibu,
Ua langu la waridi, ninakuenzi kimwana.

Japo ni mengi masafa, kukuwazia sichoki,
N'japokumbwa na maafa , moyoni mwangu hutoki,
Ninaposoma arafa, moyoni ninaafiki,
Ua langu la waridi, ninakuenzi kimwana.


Mtoto umeumbika, Rabana halaumiki,
Kisura u malaika, mannenoyo kama uki,
Hurulaini msifika, katu sina unafiki,
Ua langu la waridi, ninakuenzi kimwana.

Moyoni nitakubana, kwa aushi na mauti,
Uwe wangu wa dhamana , hata kama sina suti,
Daima tutafaaana, kwa mapenzi madhubuti,
Ua langu la waridi, ninakuenzi kimwana.

Kwa kufunga ukurasa, unalo kubwa wajibu,
Ujibari na siasa, ya nduli wasoaibu,
Kidege ninakuasa, wasome kama kitabu,
Ua langu la waridi, ninakuenzi kimwana.

Kuhitimisha shairi, nina dua kwa Khahari,
Atuepushe kiburi, na lolote lenye shari,
Lisigeuke shubiri, mapenzi na yashamiri,
Ua langu la waridi, ninakuenzi kimwana.

Hadi hapo ninatuwa, kwenda mbee nimeasi,
Maneno chukuwa, yasuke kama msusi,
Langu dau nalishuwa, memaliza ujasusi,
Ua langu la waridi, ninakuenzi kimwana.


SOLOMON OLE MUSERE,

CHUO KIKUU CHA KENYATTA.

SUBIRA.

Shairi hili nilitunga nikimwelekeza mwandani wangu,Samson Simpiri mwanagenzi wa maswala ya habari chuo cha ITI-Nairobi.

SUBIRA YAVUTA HERI .
Hujambo kaka Simpiri, sahibu mwanahabari?
Mepata wako urari, kujibu sina khiari,
Mwanetu ukae shwari, usome langu shairi ,
Mwandani stahimili, subira yavuta heri.

Mwanzo wa ngoma ni lele, msemo wa tangu kale,
Likaze sana fungule, faraja uje uole,
Muhibu katu silale, ‘dhamirayo ushikile,
Mwandani stahimili, subira yavuta heri.
 
‘Kitembea mitaani, Nairobi hapo mjini,
Uwe makini mwandani, sije ‘ingia dhikini ,
Ewe jimbi la kondeni,  huyajui ya jijini,
Mwandani stahimili, subira yavuta heri.
 
Moja siku itafika, Simpiri utatajika,
Zifazo ‘taenezeka, kama moto kwenye chaka,
Wakuite msifika, moyoni nitaridhika,
Mwandani stahimili, subira yavuta heri.
 
Nanena kweli muhibu, sipendi kukughilibu,
Dunia ina taabu,na wingi wa masaibu,
Uchunge ustaarabu, mikosi isikuswibu,
Mwandani stahimili, subira yavuta heri.
 
Kumbuka huko Nkareta, wazee tulowaata,
Mabegi tukapakata, baraste tukafuata,
Vyuoni tukajipata, weledi kuutafuta,
Mwandani stahimili, subira yavuta heri.
 
Nakuamini mwandani, ya kuwa u razini,
Mzawa wa kijijini, mtunzi mwenye imani,
Hauna maji kitwani, huna katu walakini,
Mwandani stahimili, subira yavuta heri.
 
Sahibu 'jikaze sana, uwe mja wa dhamana,
Usiwe mwenye fitina, wala mwingi wa khiana,
Na mtukufu Rabana, akuepushe laana,
Mwandani stahimili, subira yavuta heri.
 
Hapa ndipo ninatuwa, Musere ninapumuwa,
Wosia n'shautowa, na mzigo kuutuwa,
Rabuka nampa duwa, kanipa hii satuwa,
Mwandani stahimili, subira yavuta heri.

SOLOMON OLE MUSERE'
'Malenga mwitu'
CHUO KIKUU CHA KENYATTA
NOV, 2011